Nishati ya jotoardhi itakavyomaliza tatizo la umeme Tanzania

Na Lucy Samson
25 Nov 2022
Tanzania kwa sasa inatekeleza miradi mitano ya kipaumbele ya joto ardhi  ikiwemo Wilaya ya Rungwe katika maeneo ya  Ngozi  na Kiejo – Mbaka mkoani Mbeya.
article
  • Nishati hiyo iliyopo nchini inaweza kuzalisha umeme wa megawati 5,000.
  • Mikoa 16 ina rasilimali hiyo ikiwemo Mbeya
  • Ikiwa itatumiwa vizuri itasaidia kuondoa tatizo la umeme. 

Dar es Salaam. Huenda tatizo la kukatika kwa umeme likamalizika nchini mara baada ya kampuni ya Uendelezaji Jotoardhi Tanzania (TGDC) kuanza  utekelezaji wa miradi mitano ya kipaumbele ya rasilimali ya jotoardhi itakayoongeza upatikanaji wa nishati hiyo nchini. 

Kampuni   hiyo  ni kampuni tanzu  ya Shirika  la umeme Tanesco ambapo inatekeleza nishati  ya jotoardhi  inayochimbwa urefu wa kilometa  tatu kwenda chini na  ambapo rasilimali zilizopo zinaweza kuzalisha umeme wa megawati  5,000. 

Kaimu Meneja Mkuu wa  kampuni ya TGDC, Mhandisi Shakiru Kajugus alikuwa akizungumza hivi karibuni  katika ziara ya Bodi ya Wakurugenzi ya kampuni hiyo ilipotembelea  eneo la mradi lililipo  Ziwa Natron wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

 Amesema kuwa, nishati hiyo ya jotoardhi inapatikana kwa wingi katika maeneo ya bonde la ufa ambapo kwa upande wa  Ziwa Natron wapo katika hatua za utafiti kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo ambao utazalisha megawati  60 na unatarajiwa kukamilika  mwaka  2025 .

“Mradi huu wa Ziwa Natron kwa kuanzia tutazalisha megawati 10 baada ya hapo tunaendelea na upanuzi zaidi na unatarajiwa kugharimu  kiasi cha zaidi ya  Sh1 bilioni  na kukamilika kwa mradi huo  kutaleta manufaa makubwa sana kwa wananchi kwani ni nishati endelevu ya kisasa isiyotegemea mabadiliko ya tabianchi,” amesema Mhandisi Kajugus. 

 Bodi ya Wakurugenzi ya kampuni ya TGDC wakikagua mradi wa jotoardi uliopo mkoa wa Manyara.Picha|TGDC/Instagram.

Tanzania kwa sasa inatekeleza miradi mitano ya kipaumbele ya joto ardhi  ikiwemo Wilaya ya Rungwe katika maeneo ya  Ngozi  na Kiejo – Mbaka mkoani Mbeya.

Mikoa mingine ni Songwe na Pwani na tayari  ipo katika hatua ya uhakiki kwa ajili ya kuchimba visima huku kwa mkoa wa Arusha wakiendelea  na tafiti za kisayansi ambazo zinatarajiwa kumalizika mwaka 2023.

Nishati ya jotoardhi ina matumizi mengi ikiwemo kuzalisha umeme ambao hutumika kuendeshea mitambo, kupikia na kutoa mwanga majumbani.

Mwenyekiti wa bodi ya TGDC, Profesa Shubi Kaijage amesema bodi mpya wamefikia hatua ya kutembelea  moja ya miradi ya jotoardhi kujionea  na kuweza kuangalia cha  kushauri  ili mradi huo uweze  kufanyiwa kazi kwa haraka na kwa weledi.

Amesema kuwa, nishati hiyo inapatikana chini ya ardhi kwa kutumia joto lililopo  chini ya ardhi na kuwa itaweza kupunguza changamoto ya mgao wa umeme uliopo hivi sasa unaosababishwa na ukame.

“Sisi kama bodi tunaendelea kuhakikisha tunasimamia kikamilifu mradi huu ili uweze kukamilika kwa wakati na tunaomba kampuni hii iendelee kutekeleza majukumu  yake kwa wakati ili tuendelee kupata vyanzo   zaidi vya umeme,” amesema Prof Kaijage.

© Copyright 2021 JikoPoint by Nukta Africa